2016
Walinzi Juu ya Mnara
April 2016


Walinzi Juu ya Mnara

Picha
watchmen on the tower

Walinzi

Walinzi walikuwa askari wa zamu waliowekwa kwenye ukuta au ndani ya mnara ili kuweza kuchunga na kuonya kuhusu hatari zinazokaribia kutoka mbali. Waliajiriwa kulinda miji na pia mashamba ya mizeituni, mashamba, na malisho.

Aina ya Minara

Minara katika kuta za mji mara nyingi ilijengwa karibu na milango au katika kona (ona 2 Mambo ya Nyakati 26:9). Minara yote miwili ya langoni na pembeni ilitoa nafasi nzuri ya kuweza kuona hatari iliyokuwa ikikaribia na kujikinga dhidi ya mashambulizi ya adui (ona 2 Mambo ya Nyakati 26:15).

Ngome au minara ya kimbilio kawaida ilikuwa majengo yasiotegemezwa popote ambayo ilikuwa imejengwa milimani au sehemu nyingine kimkakati. Mara nyingine ilikuwa kubwa kiasi cha kuwa mahali pa mwisho pa kukimbilia kwa watu wa mji mzima walipokuwa wakishambuliwa (ona Waamuzi 9:46–52).

Minara katika mashamba ya mizeituni, mashambani au malishoni ilikuwa majengo madogo yaliyokuwa yamejengwa kwa ajili ya kulinda mimea na mifugo dhidi ya wezi na wanyama (ona 2 Mambo ya Nyakati 26:10; Isaya 5:2; 27:3). Mara nyingi, sehemu ya chini ilikuwa chumba ambacho vifaa vilihifadhiwa.

Walinzi Juu ya Mnara:

Wana mtazamo wa juu. Kama watumishi wenye mamlaka wa Mungu, manabii wametengwa kutoka mbali na dunia, wanamkaribia, na wanaruhusiwa kuona mambo kwa mtazamo wa mbinguni.

Huona mambo ambayo wengine hawawezi kuona. “Lakini mwonaji anaweza kujua vitu vilivyopita, na pia vitu vitakavyokuja, na kupitia kwao vitu vyote vitafunuliwa, kwa usahihi zaidi, vitu vya siri vitadhihirishwa, na vitu vilivyofichwa kuletwa katika nuru, na vitu visivyojulikana vitajulishwa kwao, na pia vitu ambavyo havingejulikana vitajulishwa na wao” (Mosia 8:17).

Wako macho. Manabii wana wajibu muhimu wa kutuonya kuhusu hatari inayokaribia, na wataendelea kufanya hivyo bila ya kujali maoni ya umma au mienendo katika jamii.

Wanaonya kuhusu mambo fulani yakiwa bado yako mbali na kutendeka. “Nabii hushutumu dhambi na kutabiri matokeo yake. Yeye ni mhubiri wa haki. Ikibidi, manabii waweza kuongozwa kutabiri siku za usoni kwa manufaa ya wanadamu” (Mwongozo kwa Maandiko, “Nabii,” lds.org/scriptures/gs).

Hutoa usalama na ulinzi. Kwa kutii onyo la manabii, tunaweza kupata usalama na kuepukana na misiba ambayo inaweza kutupata, binafsi au pamoja, ikiwa hatutatii.