2019
Kuvumilia Janga
Aprili 2019


Kufundisha Vijana Waliobalehe na Watoto Wadogo

Kuvumilia Janga

Picha
icons

Hivi karibuni au baadae, watoto watakabiliwa na janga, iwe ni karibu na nyumbani au mbali. Lakini “hata wakati dunia inapokuwa kwenye ghasia kote kutuzunguka, tunaweza kupokea baraka ya amani ya ndani.”1 Hapa ni baadhi ya mambo unayoweza kufanya kuwasaidia watoto kuhisi amani hiyo.

Uthabiti

Wakati janga linapotokea, watoto wanaweza kuhisi kama ulimwengu wao hauko sawa. Kuwa mfano wa uthabiti kwao. Zungumza kwa utulivu na kwa ujasiri kuhusu tukio. Endeleza utaratibu kadiri uwezavyo. Fanya kila uwezalo kuendeleza jioni ya familia nyumbani, kusoma maandiko, sala, na tabia zingine za familia. Kadiri ya muda unavyokwenda watoto wanaweza kujifunza kwamba hata wakati ulimwengu wao unatikisika, injili huleta mtazamo na maisha yanaendelea.

Heshima

Onyesha heshima katika hisia za watoto. Wasikilize watoto na tambua jinsi wanavyohisi. Waonyeshe kwamba unachukulia mambo yao kwa umakini. Wape faragha ikiwa wanaihitaji lakini waache wajue unapatikana wakiwa tayari kuzungumza. Kwa uaminifu jibu maswali pale yanapoibuka kwa kuzingatia umri walionao. Acha watoto wako wajue kwamba wanaweza siku zote kuzungumza nawe kuhusu woga na wasiwasi wao.

Mwongozo

Watoto wako wanaweza kuuliza, “Kwa nini Mungu huacha mambo mabaya yatokee?” Elezea kwamba nyakati nzuri na mbaya ni sehemu ya maisha na sehemu ya mpango wa milele wa Mungu. Anamruhusu kila mtu kufanya chaguzi zake mwenyewe, na wakati mwingine watu hufanya chaguzi mbaya ambazo husababisha maumivu. Nyakati zingine, majanga si kosa la mtu bali ni sehemu ya uhalisia. Bila kujali chochote, Baba wa Mbinguni yuko pale kwa ajili yetu. Kwa msaada wake, tunaweza kujifunza na kukua, hata kutokana na uzoefu wenye maumivu. Tunaweza kumgeukia Yeye ili kupata amani.

Uwezeshaji

Waonyeshe watoto kwamba wana nguvu ya kuleta utofauti kwa kuwapa njia ya kusaidia. Kwa mfano, wangeweza kusaidia kukusanya michango kwa ajili ya waathiriwa wa majanga, kumtembelea rafiki mgonjwa au aliyeumia hospitalini, kumpa furaha mtu anayekabiliwa na kupoteza familia, au kuwaombea wale wanaohangaika. Hatuwezi kurekebisha kila kitu, lakini tuna uwezo wa kufanya mengi mazuri, na “tunafanyia kazi amani pale tunaposaidia kutuliza mateso ya mwingine.”2

Faraja

Wakumbushe watoto wako kwamba Mungu anawapenda na kwamba wewe unawapenda. Usitoe ahadi za uwongo kwamba hakuna kitu kibaya kitakachotokea kwao, bali wahakikishie kwamba wako salama sasa na kwamba utafanya yote uwezayo kuwalinda. Wahakikishie kwamba Baba wa Mbinguni atawasaidia kupitia jaribu lolote linalokuja kwenye njia yao.

Unapojikuta umevunjwa moyo kwa jaribu, kumbuka kwamba mwishoni, mema yatashinda maovu. “Tunapigana vita dhidi ya dhambi, … lakini hatupaswi kukata tamaa,” alifundisha Rais Thomas S. Monson (1927–2018). “Ni vita ambayo tunaweza kushinda na tutashinda. Baba yetu wa Mbinguni ametupa vifaa tunavyohitaji ili kufanya hivyo. Yeye ndiye aliye katika usukani. Hatuna chochote cha kuogopa.”3

Muhtasari

  1. “Amani,” Mada za Injili, topics.lds.org.

  2. “Amani,” Mada za Injili.

  3. Thomas S. Monson, “Kuangalia nyuma na Kusonga Mbele,” Liahona, May 2008, 90.