2019
Kufanya Maamuzi: Haki ya Kujiamulia dhidi ya Ufunuo
Aprili 2019


Vijana Wakubwa

Kufanya Maamuzi: Haki ya Kujiamulia dhidi ya Ufunuo

Mwandishi anaishi Utah, Marekani.

Linapokuja suala la maamuzi makubwa, ni kwa kiasi gani tunahitaji kumtegemea Mungu kutuambia nini cha kufanya?

Picha
woman standing in front of river

Vielelezo na David Green

Kila siku kila mmoja wetu hukutana na maamuzi mengi. Baadhi ni ya kidunia, kama, “Ni nini napaswa kuvaa?” “Nini napaswa kula kwa ajili ya chakula cha mchana?” “Je, ni muda wa kununua gari mpya, au naweza kubaki na ya zamani kwa muda mrefu kidogo?” Lakini mara nyingi kila mara tunakutana na uamuzi mkubwa—“Je, ninapaswa kurudi shule?” “Je ninapaswa kuikubali kazi hii?” “Je, ninapaswa kuhamia katika jiji jipya?” “Je ninapaswa kununua nyumba?” “Je ninapaswa kwenda miadi na mtu huyu?” “Je ninapaswa kufunga ndoa na mtu huyu?” na kadhalika.

Tunapokabiliwa na maamuzi makubwa, tunajaribu—kwa usahihi—kuchukua muda mrefu kufanya uchaguzi. Tunafuata ushauri uliotolewa kwa Oliver Cowdery katika Mafundisho na Maagano 9:8–9, ambapo Bwana anasema:

“Lakini, tazama, ninakuambia, kwamba unalazimika kulichunguza katika akili yako; ndipo uniulize kama ni sahihi, na kama ni sahihi nitaufanya moyo wako uwake ndani yako; kwa njia hiyo, utahisi kuwa hiyo ni sahihi.

“Lakini kama siyo sahihi hutapata hisia za namna hiyo, bali mzubao wa mawazo ambayo yatakufanya usahau kitu kile kisicho sahihi.”

Japokuwa huu hakika ni ushauri mzuri, linapokuja suala la maamuzi makubwa, wakati mwingine tunategemea kwa kiasi kidogo sana sehemu ambayo Mungu hutuambia kile kilicho sahihi na si vya kutosha kwenye sehemu ambapo Yeye hutuambia kulichunguza katika akili zetu. Tunakwama tukisubiri Mungu kuthibitisha maamuzi yetu kiasi kwamba tunaacha fursa nzuri zitupite. Tunaweza hata kutambua kazi ya haki ya kujiamulia, lakini tunaogopa kufanya uamuzi ambao unaweza kututoa kwenye njia kutoka kwenye “mpango” wetu uliobainishwa kabla na kuishia kukisia kwamba chochote zaidi ya mwako wa moyo au sauti kutoka mbinguni humaanisha kwamba uchaguzi wetu ni mbaya. Kwa wengi wetu, mvuto huu usioelezeka kati ya haki ya kujiamulia na ufunuo binafsi huongoza kwenye swali moja la muhimu: Ni nini wajibu wa Mungu katika kutusaidia kufanya maamuzi?

Wajibu wa Mungu katika Kufanya Uamuzi

Pengine swali hili linaweza kujibiwa vizuri kupitia hadithi ya kaka wa Yaredi. Kuna mpangilio wa kuvutia wa ukuaji katika hadithi hii ambao unatufundisha kuhusu jinsi Mungu anavyotarajia tufanye maamuzi. Baada ya lugha kuchanganywa kwenye Mnara wa Babeli, Yaredi anamuomba kaka yake kumuuliza Bwana ikiwa walipaswa kuondoka, na kama ndivyo, wapi walipaswa kwenda (ona Ether 1:36–43). Kaka ya Yaredi anauliza, na Bwana anawaongoza kwenye ufuko wa bahari. Wanaposafiri, Bwana anazungumza nao katika wingu na kuongoza kila hatua ya safari yao. Hatimaye wanafika ufukoni mwa bahari, ambapo wanakaa kwa miaka minne.

Mwishoni mwa miaka minne, Mungu anamwambia kaka wa Yaredi kujenga mashua na kuwa tayari kuvuka bahari. Wakati kaka wa Yaredi anagundua merikebu hazikuwa na hewa, anafuata mpangilio uleule wa kwenda kwa Mungu kumuuliza kile anachopaswa kufanya. Kama ilivyotarajiwa, Bwana alijibu kwa kumpa maelekezo ya kina kutengeneza matundu upande wa juu na chini wa merikebu. Gundua mpangilio wa ufunuo mpaka sasa: Mungu anawapa mpango, wanauliza maswali kuhusu jinsi ya kutimiza mpango, na Mungu anajibu kwa majibu ya kina na ya uhakika.

Baada ya kutengeneza matundu kwenye merikebu, kaka wa Yaredi anagundua kwamba merikebu hazitakuwa na mwanga. Kwa mara nyingine tena anamuuliza Mungu ni nini angepaswa kufanya. Badala ya kujibu, hata hivyo, Mungu anauliza—“Ungetaka nifanye nini ili muwe na mwangaza kwenye mashua yenu?” (Etheri 2:23). Badala ya kutoa maelekezo ya kina kama Alivyofanya kabla, wakati huu Bwana anamsubiri kaka wa Yaredi kuamua nini cha kufanya.

Aina hii ya jibu kutoka kwa Bwana pengine ni gumu kulielewa wakati wa kujaribu kufanya uamuzi. Tunafundishwa kuomba na kusubiri jibu, hivyo kiuhalisia tuna wasiwasi tunapokosa jibu. Mara nyingi tunajiuliza ikiwa ukosefu wa jibu la wazi unakidhi kuwa “mzubao wa mawazo” ukionyesha kwamba uchaguzi wetu ni mbaya. Wakati mwingine tunajiuliza ikiwa inamaanisha hatuko waadilifu vya kutosha kusikia jibu au ikiwa hatuombi kwa “kusudi halisi” (ona Moroni 10:4). Lakini kuna njia ya tatu ambayo wakati mwingine hatuifikirii—pengine, kama vile kwa kaka wa Yaredi, Mungu anasubiri sisi tufanye uamuzi wetu wenyewe

Kufanya Uamuzi

Hivi karibuni nilikutana na hali ambayo ilitoa changamoto kwa jinsi nilivyofikiria kuhusu haki ya kujiamulia na ufunuo binafsi. Nilipokuwa nakaribia mwisho wa kuhitimu, nilipata nafasi tofauti za kazi katika majiji tofauti na nisingeweza kuamua ipi ya kuchukua. Kama kaka wa Yaredi, nilikuwa nimepitia uzoefu wa nyakati nyingi ambapo nilikuwa nimesali kuhusu uamuzi mkubwa na Mungu alijibu kwa jibu lenye uhakika. Kwa kutegemea uzoefu huo wa mwanzo, nilianza kumuomba Mungu anisaidie kuamua ni kazi gani ningechagua. Nilikuwa pia nikifanya sehemu yangu kwa kujifunza kuhusu kila nafasi ya kazi na kushauriana na watu wengi. Lakini bila kujali ni kwa kiasi gani niliomba, mbingu zilikaa kimya, na sikupokea jibu.

Picha
two different cities

Tarehe ya mwisho ya kufanya maamuzi ilikaribia, na nilianza kupata wasiwasi. Hakika huu ulikuwa ni uamuzi Bwana alipaswa kuujali, hivyo kwa nini Hakujibu? Pengine hakujali kuhusu kazi ipi nilichagua, lakini lazima ajali kuhusu ni jiji lipi nilihamia kwani ingekuwa na matokeo kwenye maisha yangu. Bwana daima alikuwa akijali kuhusu maamuzi yangu huko nyuma, hivyo kwa nini Asingejali kuhusu huu pia?

Hata hivyo bila kujali nilijaribu kwa kiasi gani, hakuna jibu lililokuja. Nilianza kujiuliza ikiwa nilikuwa nimesonga mbali kutoka kwa Mungu kiasi kwamba sikuweza kusikia jibu Lake. Nilijiuliza pia ikiwa nisingeweza kusikia kwa sababu bila kufahamu sikutaka kusikia jibu. Hatimaye, siku moja kabla ya tarehe ya mwisho, nilijua nilipaswa kufanya uamuzi, hivyo nilitumia busara yangu na kufanya uamuzi. Usiku ule niliomba, nikiuliza ikiwa Yeye angeniambia kama jibu langu halikuwa sahihi. Bado jibu halikuja, hivyo niliamua kuikubali kazi.

Miezi kadhaa baadaye, nilikuwa bado na mashaka na uamuzi wangu, hivyo niliomba baraka ya ukuhani ili kuwa na uhakika. Katika baraka niliambiwa kwamba sikupata jibu la ombi langu kwa sababu Bwana alikuwa na furaha kwa uamuzi wowote ambao ningefanya. Baraka hii iliimarisha ushauri niliopewa kabla na rais wangu wa misheni, ambaye aliniambia kwamba mara nyingi haijalishi ni uamuzi gani tunafanya. Mungu anatutaka tujifunze jinsi ya kusimama kwa miguu yetu miwili na kuamua jinsi ya kuishi maisha yetu. Rais wangu wa misheni pia alinikumbusha kwamba Mungu, kama Baba yetu wa Mbinguni, hatatuadhibu na kutuondolea fursa zilizoahidiwa ikiwa kwa dhati tunajaribu kuamua nini cha kufanya.

Kaka wa Yaredi vilevile angeweza kupendekeza karibia suluhisho lolote kupata mwanga kwenye mashua, na Bwana angelikubali. Kiwango cha uzoefu kilikuwa siyo tu kwa kaka wa Yaredi kuimarisha imani yake bali pia kujifunza kufanya uamuzi.

Kutumia Haki ya Kujiamulia

Picha
different paths

Kutoka kwenye mtazamo wa milele, kutumia haki ya kujiamulia ni sehemu muhimu ya ukuaji binafsi. Bila kuwa nayo, hatuwezi kufanya aina ya maamuzi ambayo yatatusaidia kufikia uwezekano wetu mkamilifu. Ukuaji, sawa na kila kitu katika injili, huja mstari juu ya mstari, kanuni juu ya kanuni” (2 Nefi 28:30). Mungu anatutaka tuwe watu waliojiandaa, siyo watu waliopooza, na Yeye anatarajia sisi kutumia haki yetu ya kujiamulia kuishi maisha yetu vizuri kadiri tuwezavyo.

Tukiweza kujifunza kutafuta usawa kati ya haki ya kujiamulia na ufunuo, tunaweza kupata ukuaji wa kweli kiroho. Hiki ndicho kilichotokea kwa kaka wa Yaredi. Baada ya kutafakari, alifanya kazi kuyeyusha mawe 16 kutoka kwenye mwamba na kumuomba Mungu kuyagusa na kuyafanya yatoe mwanga (ona Etheri 3:1–5). Wakati huu, wakati Mungu alipojibu, kila kitu kilibadilika. Badala ya kusikia sauti ya Bwana mawinguni, kaka wa Yaredi hasa alimwona Bwana, ambaye siyo tu alitokea Yeye mwenyewe lakini pia alimwonyesha kaka wa Yaredi maono ya kustaajabisha ya ulimwengu na kila kitu ambacho kingekuja (ona Etheri 3:6–26). Inawezekana kwamba kaka wa Yaredi asingekuwa ameandaliwa kiroho kupokea ono lile kama kwanza asingepata uzoefu wa ukuaji binafsi ambao ulikuja kutokana na kufanya uamuzi wake mwenyewe.

Tunapofanya maamuzi, tunapaswa kwa hakika kufuata ushauri wa Alma wa “kushauriana na Bwana kwenye matendo [yetu] yote” (Alma 37:37). Wakati Bwana anatuhitaji tufanye uamuzi fulani, Yeye atatujulisha na kusaidia kutuzuia kutokwenda mrama. Lakini pia lazima tujiandae kusimama na kusonga mbele kwa imani, bila kujali jibu linakuja au la. Ili mradi tunatunza maagano yetu na kubaki waaminifu kwenye injili ya Yesu Kristo, tunaweza kuhisi ujasiri katika maamuzi yetu ya haki na amani kwamba Bwana ameridhishwa na juhudi zetu.