2019
Masomo matatu juu ya Upendo, Shangwe, na Amani
Aprili 2019


Masomo matatu juu ya Upendo, Shangwe, na Amani

Kutoka kwenye hotuba ya mkutano wa ibada, “Furaha, Uwongo, na Mambo Madogo,” iliyotolewa katika Chuo Kikuu cha Brigham Young mnamo Novemba 5, 2017.

Kufuata hatua hizi tatu kunaweza kuleta tofauti kubwa katika maisha yako na kukusaidia kuhisi matunda ya Roho.

Picha
bowl of fruit

Nilipokuwa mwanafunzi wa chuo, niliwaza sana kuhusu siku zangu za mbeleni. Nilipofika kwenye siku hizo—nikimaanisha maisha baada ya chuo—nilijifunza masomo muhimu matatu ambayo yalileta tofauti kubwa katika maisha yangu. Ninataka kushiriki nanyi masomo haya kwa tumaini kwamba hamtachukua muda mrefu kama niliochukua kujifunza masomo hayo. Yanaweza kuwasaidia kupata shangwe tele katika maisha—na hatimaye kupata kuinuliwa na Baba yenu wa Mbinguni.

1. Tafuta Furaha, Amani, na Roho Mtakatifu

Nilikutana na mke wangu, Melinda, wakati nikiwa mwanafunzi wa mwaka wa pili chuoni, takribani miezi sita baada ya kurudi kutoka kwenye misheni yangu. Nilijua mara moja kwamba nilitaka kumuoa Melinda. Melinda, hata hivyo, hakuwa na uzoefu sawa na wangu. Haikuwa hivyo mpaka miaka mitano baadaye kwamba hatimaye alipokea jibu kwamba ilikuwa “SAWA” kama angeolewa nami.

Katika kipindi hicho cha miaka mitano, nilipata moja ya jaribu zito zaidi la maisha yangu. Nilijua nani nilipaswa kumuoa, na Roho alinisihi sana, lakini sikuonekana kufikia lengo hilo.

Muda mfupi baada ya kuhitimu, Melinda aliamua kwenda misheni—kwa sehemu, nashawishika, alitaka kuwa mbali na mimi. Kulikuwa na nyakati wakati akiwa katika misheni yake nilipokuwa na huzuni kwa sababu nilifokasi kwenye kile nilichokosa. Hata hivyo, nilikuwa nikisoma maandiko na kusali kila siku, kutumikia Kanisani, na kujitahidi kufanya mambo yaliyomkaribisha Roho Mtakatifu katika maisha yangu.

Mapema, asubuhi ya Jumapili moja yenye baridi sana huko Minneapolis, Minnesota, Marekani, nilipokuwa nikiendesha gari kwenda kwenye mkutano wa Kanisa, niliwaza, “ninapaswa kuwa mwenye huzuni sana muda huu. Hakuna kilichoonekana kwenda jinsi nilivyotaka. Lakini sina huzuni. Ninahisi furaha isiyoelezeka!”

Sasa, ni kwa jinsi gani ningeweza kuwa na furaha kama nilikuwa napitia kile, ambacho kwangu, kilikuwa jaribu zito?

Jibu linapatikana katika Wagalatia 5:22–23: “Tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, upole, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi.”

Kwa sababu nilikuwa nikifanya mambo yanayomwalika Roho katika maisha yangu, nilihisi upendo wa Mungu. Nilihisi furaha na amani. Ningeweza kuteseka kwa muda mrefu na bado kuwa na furaha.

Kuwa na upendo, furaha, na amani katika maisha yetu, familia zetu, na ndoa zetu hakuji kutokana na kuwa na nyumba kubwa, gari nzuri, nguo zilizo kwenye fasheni, mafanikio ya kazi, au lolote kati ya mambo mengine ulimwengu unayosema yanaleta furaha. Kwa kweli, kwa sababu hisia za upendo, furaha, na amani huja kutoka kwa Roho, kuzihisi hakuhitaji kuhusisha hali zetu za kimwili kabisa.

Tafadhali eleweni kuwa sisemi kwamba daima tutakuwa na furaha au kwamba hali zetu za kimwili kamwe haziathiri furaha yetu. Kwa kweli, kama hatuonji uchungu, hatuwezi kujua utamu (ona Mafundisho na Maagano 29:39; ona pia Musa 6:55).

Tunahitaji kuteseka wakati mwingine. Zaidi ya hayo, baadhi ya hali za kimwili na kihisia zinaweza kutusababishia mateso mazito na kufanya iwe vigumu kwetu kuhisi Roho. Lakini ikiwa tunajitahidi kuwa na Roho katika maisha yetu na tunamwamini Mungu, tunaweza, kwa ujumla, kuwa na furaha.

Ninashuhudia kutokana na uzoefu binafsi kwamba hii ni kweli. Tangu uzoefu wangu wakati Melinda akiwa kwenye misheni yake, nimegundua kwamba kama ninafanya mambo yanayomwalika Roho katika maisha yangu, ikijumuisha kuchagua kuamini na kukubali kwamba mambo yataenda sawa kama Mungu anavyokusudia, daima ninakuwa na furaha (ona Yakobo 3:2).1

Usiangukie kwenye Kisicho Halisi.

Picha
bowl of fake fruit

Shetani anatoa kisicho halisi kama mbadala wa yote Mungu anayofanya ili kujaribu kutukanganya na kutudanganya. Licha ya juhudi za shetani kutushawishi vinginevyo, Mwokozi anatufundisha kwamba “mti mbaya [hauwezi] kuzaa matunda mema” (3 Nefi 14:18). Kwa sababu shetani ni mti mbaya, hawezi kutusababisha kuhisi “upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, [na] kiasi” (Wagalatia 5:22–23). Badala yake, Shetani anataka kutufanya wenye huzuni (ona 2 Nefi 2:27).

Basi ni nini Shetani anafanya? Anajaribu kutudanganya.

Rafiki yangu, mmoja wa wateule, alidanganywa. Rafiki yangu alitumikia misheni na alikuwa mmisionari wa kufana. Aliporudi nyumbani kutoka kwenye misheni yake, alikusudia kufanya mambo madogo yote ambayo yalimwalika Roho katika maisha yake na yaliyomuimarisha katika misheni yake. Na kwa muda, alifanya.

Hata hivyo, aliwaona marafiki, wengi wao wakiwa wamisionari waliorudi, wakija kanisani kila jumapili lakini nje ya kanisa wakiishi kama ulimwengu ulivyoishi. Walionekana wenye furaha. Walikuwa wakifanya vitu vyenye kuleta “kuchangamsha”. Na mtindo wao wa maisha haukuonekana kuhitaji juhudi kubwa kama yake ilivyohitaji.

Taratibu aliacha kufanya mambo madogo madogo ambayo yalikuwa yamemletea nguvu ya kiroho kwenye misheni yake. Bado alikuwa na ushuhuda, lakini aliniambia kwamba alikuwa amehitimisha, “Kama nilikuwa nahudhuria tu mikutano yangu ya Kanisa, nilikuwa SAWA—nilikuwa kwenye njia.” Hata hivyo, alisema, “Kiroho, nilikuwa mlegevu.”2 Pale alipoishi kama ulimwengu ulivyoishi, uchaguzi mmoja mbaya ulipelekea mwingine, na punde akapata ujauzito.

Chaguzi zake zisizo za haki hatimaye zilimnasa. Hakuwa na furaha, na alijua hilo. Kwa bahati nzuri, rafiki yangu aligundua kwamba alikuwa amedanganywa, na alitubu.

Hadithi yake inasisitiza kwamba hata walio bora kati yetu wanaweza kudanganywa. Zaidi ya hayo, hadithi yake inaonyesha kwamba lazima siku zote tuweke ulinzi dhidi ya udanganyifu. Tunafanikisha hili kwa kufanya mambo madogo ambayo humwalika Roho katika maisha yetu.

Nina furaha kusema kwamba leo rafiki yangu ni mwenye furaha, anajitahidi kutii amri, na yuko hai kimwili na kiroho katika injili.

Udanganyifu wa Shetani huja kwa njia nyingi. Nitataja chache tu.

Shetani hujaribu kutushawishi kuyapa kipaumbele mambo ya muda kuliko mambo ya kiroho. Tunaweza kuona kama vipaumbele vyetu si vya kiroho kwa kugundua mara nyingi kiasi gani tunasema, “nina shughuli nyingi au nimechoka sasa hivi ku _________.” Jaza nafasi iliyo wazi: kuhudhuria hekaluni, kuhudumu, kujifunza na kutafakari maandiko, kutimiza wito wangu, au hata kuomba.

Sababu moja ya sisi kuhisi tuna shughuli nyingi ni kwamba Shetani anafanya kazi kwa bidii kutuvuruga. Anatumia simu viganjani mwetu, redio ndani ya gari zetu, televisheni nyumbani mwetu, na vitu vingine vingi kutufanya tuvurugwe karibu kila wakati. Kama matokeo, tunahisi tuna shughuli nyingi kuliko ilivyo hasa.

Matokeo mengine ya uvurugaji huu ni kwamba tunatafakari kidogo sana. Shetani anafanya kazi kutuvuruga kwa sababu anajua kwamba kutafakari, hasa maandiko, hupelekea uongofu mkubwa na ufunuo.

Lingine la udanganyifu wa Shetani huja kupitia wazo kwamba matendo yetu ya nje yana maana sana kuliko msukumo wa ndani. Wakati tunapokosa msukumo sahihi wa kufanya mambo ya kiroho, tunashindwa kupata uzoefu wa shangwe ya injili. Kama matokeo, kutii amri kunaanza kuonekana kama kazi ngumu, na shetani anajua kwamba kama akifanikiwa kutufanya tuhisi hivi, kuna uwezekano wa kuacha kufanya kile tunachojua tunapaswa kufanya.

Shetani pia anatudanganya kwenye kuamini kwamba shangwe na furaha vinakuja kutokana na kuwa na maisha rahisi au kwa kuburudika tu wakati wote. Haviji kwa namna hiyo. Ukweli ni kwamba hakuna shangwe au furaha bila kitu cha kushinda (ona 2 Nefi 2:11, 23).

La mwisho kati ya udanganyifu wa Shetani nitakalolitaja ni kwamba anajaribu kutushawishi kwamba uovu, na burudani yake ya muda mfupi, kweli ni furaha. Shetani anajua kwamba, angalau kwa muda, hisia fulani zinaweza (1) kutufanya tudhani kwamba tunahisi matunda ya Roho, (2) kutuvalisha kinyago cha matamanio yetu kwa matunda hayo, au (3) kuhisi kama mbadala unaokubalika.

Kwa mfano, Shetani anaweza kutujaribu sisi tutafute matamanio kwenye nafasi ya upendo. Anaweza kutuvutia kwa furaha badala ya shangwe ya kudumu. Anajaribu kutuvuruga kuliko kutupatia amani. Angetufanya tuwe wenye kujisikia wenye haki katika macho yetu wenyewe, wenye ari, na sahihi kisiasa badala ya kutokuwa wabinafsi, watiifu daima, na wenye fokasi ya kiroho inayofaa. Majaribu yake yanaweza kutusababisha kuchanganyikiwa, ambayo huweza kutupelekea kufikiri kwamba kutokutii amri kutaleta furaha.

3. Fanya Mambo Madogo

Kwa kawaida ni mambo madogo ambayo humleta Roho katika maisha yetu, hutulinda dhidi ya kudanganywa, na hatimaye hutusaidia kupata nguvu ya kutii amri na kupata uzima wa milele. Mwokozi alifundisha kanuni hii kwa wazee wa Kanisa huko Kirtland, Ohio: “Kwa hiyo, msichoke kutenda mema, kwa kuwa mnaijenga misingi ya kazi kubwa. Na kutokana na mambo madogo huja yale yaliyo makuu” (Mafundisho na Maagano 64:33).

Kwa nini mambo madogo ni muhimu sana? Katika mstari unaofuata, Mwokozi alielezea kwamba “Bwana anahitaji moyo na akili yenye kukubali” (Mafundisho na Maagano 64:34). Kwa nini Mwokozi aliunganisha kufanya mambo madogo na moyo na akili yenye kukubali? Kwa sababu kwa kuendelea kufanya mambo madogo, tunaiweka mioyo na akili zetu kwa Mungu, ambako kunatusafisha na kututakasa (ona Helamani 3:35.)

Kusafishwa na kutakaswa huku hubadilisha asili yetu hasa, kidogo kidogo, ili kwamba tuwe zaidi na zaidi kama Mwokozi. Hii pia hutusababisha kuwa wasikivu zaidi kwa msukumo wa Roho Mtakatifu, ambao hutufanya tuwe na uwezekano mdogo wa kudanganywa.

Katika mwaka wangu wa shule ya upili, baba yangu alinifundisha seminari nyumbani kwetu. Kwa sababu mada ya mwaka ule ilikuwa Kitabu cha Mormoni, baba yangu aliamua kwamba tungekisoma pamoja, mstari kwa mstari, na kujadili kile tulichojifunza. Tuliposoma, baba yangu angeuliza maswali ambayo yalinifanya nifikirie kuhusu kile tulichokuwa tunasoma, na angefafanua mambo ambayo sikuyaelewa. Bado nakumbuka kujifunza kuhusu Mwokozi na kuhisi kwamba kweli aliwatembelea Wanefi na kwamba kweli ningeweza kusamehewa dhambi zangu kwa sababu ya Upatanisho Wake.

Ninafuatisha msingi wangu katika maandiko kwenye vikao vile mimi na baba yangu tulivyokuwa navyo pamoja. Nilihisi kitu tuliposoma. Na pengine muhimu zaidi, matamanio yangu, sababu ya kufanya jambo, na matendo vilibadilika. Nilitaka kuwa mzuri zaidi. Nilianza kuona wapi nilikuwa nikidanganywa. Nilitubu kile mara. Mwishoni mwa mwaka wangu wa mwisho chuoni, nilikuwa nikisoma maandiko kila siku.

Katika wakati huu, Rais Ezra Taft Benson (1899–1994) aliwaomba waumini wa Kanisa kusoma Kitabu cha Mormoni kila siku na kufanyia kazi kile walichojifunza.3 Hivyo, kwa kuongezea kwenye kingine nilichokuwa nikisoma, nilisoma angalau kitu kutoka kwenye Kitabu cha Mormoni.

Picha
fruit and scriptures

Kwenye misheni yangu nilijifunza jinsi ya kusoma hasa na kusherehekea maandiko. Siyo tu nilihisi Roho Mtakatifu niliposoma, bali pia nilianza kuhisi shangwe nilipoyapekua maandiko kutafuta majibu kwa matatizo yangu na yale ya watu niliokuwa nikiwafundisha.

Baada ya misheni yangu, niliendelea kusherehekea maandiko kila siku. Kwa sababu utamaduni huu ulialika Roho Mtakatifu kwenye maisha yangu, nilipokea mwongozo Wake kunisaidia kutumia muda wangu kwa ufanisi zaidi. Kama matokeo, nilifanya vizuri shuleni na, baadaye, kazini. Ilikuwa rahisi kufanya chaguzi nzuri. Niliomba zaidi na nilikuwa mwenye bidii zaidi katika kutimiza miito yangu. Kusherehekea maandiko kila siku hakukutatua matatizo yangu yote, lakini maisha yalikuwa rahisi.

Mnamo Agosti 2005, Rais Gordon B. Hinckley (1910–2008) alitoa changamoto ya kusoma au kusoma kwa mara nyingine Kitabu cha Mormoni kabla ya mwisho wa mwaka.4 Kwa sababu nilikuwa nikisoma kutoka kwenye Kitabu cha Mormoni kila siku, nilikuwa tayari kwenye Etheri au Moroni. Kwa hiyo, baada ya kumaliza wiki moja au mbili baadaye, nilihitimisha kwamba nilikuwa nimemaliza changamoto ya Rais Hinckley.

Lakini kisha mwalimu wa nyumbani mwaminifu alikuja kutembelea familia yetu. Aliniuliza maendeleo yangu kwenye mwaliko wa Rais Hinckley.

Nilimwambia kwamba nilikuwa na bahati nzuri ya kuanza Kitabu cha Mormoni kabla ya changamoto ya Rais Hincley. Kisha, kwa kujipa haki, nilitangaza kwamba nilikuwa nimemaliza jukumu.

Kwa bahati nzuri, mwalimu wangu wa nyumbani aliona mambo kitofauti. Pale taratibu aliponisahihisha, Roho alininong’oneza kwamba mwalimu wangu wa nyumbani alikuwa sahihi.

Sasa nilitakiwa kusoma sura mbili kila siku ili kumaliza tena ifikapo mwisho wa mwaka. Nilipoongeza kasi ya kusoma katika Kitabu cha Mormoni, niligundua kwamba hata nguvu zaidi ilikuja katika maisha yangu. Nilikuwa na shangwe zaidi. Niliona mambo kwa uwazi zaidi. Nilitubu mara nyingi zaidi. Nilitaka kuwatumikia na kuwaokoa wengine. Sikuweza kuathirika kirahisi na udanganyifu na majaribu ya Shetani. Nilimpenda Mwokozi zaidi.

Novemba ile niliitwa kuwa askofu wa kata yetu. Kukamilisha changamoto ya Rais Hinckley kuliniandaa kwa wito huo. Tangu hapo, nimegundua kwamba kadiri ninavyokuwa na shughuli nyingi iwe kazini au kanisani, ndivyo zaidi ninahitaji kusoma maandiko, hasa Kitabu cha Mormoni.

Unaweza kuwa na baraka na nguvu sawa na hiyo katika maisha yako ikiwa nawe pia utasherehekea maandiko kila siku. Ninaahidi kwamba ikiwa utasherehekea maandiko kila siku, hasa Kitabu cha Mormoni, utamwalika Roho kwenye maisha yako na kiuhalisia utaomba kila siku, utatubu mara nyingi zaidi, na kuona ni rahisi kuhudhuria kanisani na kupokea sakramenti kila wiki.

Ninashuhudia kwamba unapofanya mambo madogo na kumwamini Bwana, unaweza kupata upendo, shangwe, amani, na furaha bila kujali hali zako. Ninashuhudia pia kwamba hii imewezekana kwa sababu ya dhabihu ya Yesu Kristo. Kila kitu kizuri huja kwa sababu Yake (ona Moroni 7:22, 24).

Muhtasari

  1. Tunapokuwa imara katika imani ya Kristo, tunaweza kusherehekea upendo wa Mungu bila kujali hali zetu.

  2. Muhtasari na nakala ya usahili katika umiliki wa mwandishi.

  3. Ona Ezra Taft Benson, “Jukumu Takatifu,” Ensign, Mei 1986, 77–78; ona pia “Kitabu cha Mormoni—Jiwe Kuu la Tao la Dini Yetu,” Ensign, Nov. 1986, 4–7.

  4. Ona Gordon B. Hinckley, “Ujumbe waUrais wa Kwanza: Ushuhuda wa Kusisimua na wa Kweli,” Ensign, Agosti. 2005, 2–6.