2020
Kumsaidia Mama yangu kwenye safari yake ya kushinda Uraibu
Oktoba 2020


Kidijitali Pekee: Vijana Wakubwa

Kumsaidia Mama yangu kwenye safari yake ya kushinda Uraibu

Sio rahisi, lakini kutembea njia ya uponyaji pamoja na wale wanaopambana na uraibu ni jambo la kufaa.

Kufikia wakati nilipokuwa mkubwa vya kutosha kuelewa pombe ni nini, nilijua mama yangu alikuwa na shida nayo. Wanafamilia walijaribu kunificha mimi na dada yangu suala lake, lakini waliweza tu kuficha ulevi wa mapema asubuhi na kuumwa kichwa kwa muda mrefu.

Mama yetu alikuwa mlevi—na hakuna kisingizio au hadithi ya uchanganuzi ambayo ingeweza kubadilisha hilo.

Kama msichana mdogo, niliamini kwamba uraibu ni chaguo. Nilihisi kuchoshwa kila wakati mama yangu alipopita mlangoni kwetu na harufu ya pombe kwenye pumzi yake baada ya kuahidi kuacha ulevi. Ilikuwa ni kama hataki kubadilika. Lakini miaka ya machozi yake yenye uchungu, majaribio yaliyoshindwa, na kuporomoka kwa afya vilinifundisha vinginevyo.

Nilipokuwa katika shule ya upili, nilianza kugundua kuwa uraibu wa mama yangu “usingefika kikomo kwenye usiku ule wa kupendeza,” kama mshairi Dylan Thomas wakati mmoja alivyoandika1—na sio kwa sababu hataki kubadilika. Haikuwa kuhusu ukosefu wa nguvu ya utayari kwa sehemu yake au kwamba alikuwa akichagua pombe juu ya familia yake. Alikuwa amenaswa katika uraibu wake.

Kama Rais Russell M. Nelson alivyoelezea: “Uraibu unasalimisha uhuru wa kuchagua wa baadaye. Kupitia njia za kikemikali, mtu anaweza kiuhalisia kutengwa kutoka kwenye mapenzi yake mwenyewe!”2 Kupata uponyaji ingekuwa vita kati ya mwili wake na roho yake kwa miaka ijayo.

Kuvumilia Mzunguko wa Kurudia Uraibu

Baada ya kutimiza miezi sita ya kushinda uraibu, nilianza kumtambua mama yangu tena—yule ambaye alikuwa akidensi kwenye gari na kuandika mashairi mazuri na kuwaambia marafiki zangu utani wa kuaibisha. Ilikuwa ni kama mtu nyuma ya pazia ghafla aliwasha tena taa kwenye macho yake na alikuwa akifanya kazi muda wa ziada ili kuifanya iendelee kuwaka. Hakuwahi kushinda uraibu kwa muda mrefu hivyo katika miaka mingi, na ilikuwa ya kupendeza kumpata tena.

Lakini haikudumu. Usiku mmoja, kabla ya kupata nafasi ya kuongea, mimi na dada yangu tulijua. Macho yake yaliyong’aa na mashavu yaliyojaa yalisema yote: baada ya miezi sita na siku nne, alikuwa amerudia uraibu. Kwa muda mfupi, tulifikiria kutoka nje, mbali na wasiwasi na hofu, lakini tulijua kwamba alitaka kubadilika. Hatungeweza kumfanyia hilo kwa niaba yake, lakini tungeweza kumsaidia wakati akitembea njia ya uponyaji.

Kuvunja Ukimya wa uraibu

Katika miezi michache iliyofuata, mimi na dada yangu tulitafuta njia za kumsaidia mama yangu kuendelea kusonga mbele kufikia kushinda uraibu kwa muda mrefu. Haingekuwa rahisi, lakini alikuwa amewahi kufanya hilo, na tulijua angeweza kulifanya tena.

Nikiwa nimemshuhudia mama yangu akirejea unywaji pombe hapo awali, tulijua nini cha kutarajia, kwa hivyo tulikusanya chupa zote za pombe na divai ambazo tungeweza kupata na kuzitupa chini kwenye mfereji. Kisha tukachukua shehena ya kinywaji cha Gatorade kwenye duka na kusafisha nyumba; lilikuwa jaribio letu bora kumuondoa mama yangu kutoka kwenye mazingira ambayo alikuwa ndani yake wakati aliporudia uraibu.

Baada ya siku chache, mama yangu alikuwa mzima vya kutosha kurudi kazini, lakini tulijua mapambano hayajamalizika. Hadi kufikia hatua hiyo, kina cha uraibu wake kilifichwa kutoka kwa wanafamilia na marafiki wengi. Kwa miaka mingi, ilikuwa jambo la siri—chanzo cha aibu, kitu ambacho mtafiti wa sayansi ya jamii Brené Brown anaelezea “hupata nguvu yake kutoka kwenye kutozungumziwa.” Ikiwa tulitaka yeye aendelee kubaki ameshinda uraibu, tulihitaji kuvunja ukimya.

Kuamua kuwa wawazi kwa familia yetu na marafiki wengine wa kuaminika ilikuwa vigumu, lakini pia ilikuwa yenye kuleta ukombozi. Aibu “huharibu sehemu yetu hasa ambayo inaamini tunaweza kubadilika na kufanya vizuri,”4 kwa hivyo kitendo hasa cha kuzungumza juu ya uraibu wake kilimpa mama yangu (na mimi!) tumaini tena. Hatukuwa peke yetu, na kwa mara ya kwanza katika miaka mingi, tulianza kupata picha ya maisha yasiyotawaliwa na uraibu wake.

Kushikilia Tumaini

Sitajaribu kuipaka sukari: kudumisha tumaini si rahisi kila wakati. Kwa miaka mingi nilimuunga mkono mama yangu wakati akijaribu kushinda uraibu, lakini nitakuwa nasema uwongo ikiwa nitasema sikupata huzuni, kukata tamaa na mfadhaiko njiani. Akizungumzia safari ngumu ambayo mtu anaikabili ili kushinda uraibu, Rais Nelson alielezea: “Kila mtu anayeamua kupanda barabara hiyo ya mwinuko kuelekea uponyaji lazima ajiunge kwenye mapambano ya maisha yote. Lakini maisha yote ni tuzo inayostahili gharama hiyo.”5

Kama umewahi kumpenda mtu ambaye anajitahidi kupambana na uraibu, unajua ni vigumu kiasi gani inavyokuwa kuwaona wakijiangamiza wenyewe. Lakini hata baada ya kuamka kutoka kwenye kurudia uraibu, tumaini halipotei kamwe. Kwa sababu ya dhabihu Yake ya upatanisho, Mwokozi anajua “jinsi ya kutusaidia [sisi] kulingana na unyonge [wetu]” (Alma 7:12). “Akiwa na uponyaji katika mabawa yake” (3 Nefi 25:2), Anatunyanyua pale tunapojihisi tumechoka kuendelea mbele, “anatubeba na kututia moyo, akikataa kutuachilia mpaka tufike nyumbani salama.”6

Kwa hivyo iwe umechukua hatua yako ya kwanza tu au umesafiri maili elfu moja na mtu kwenye safari yao ya uponyaji, hapa kuna mambo kadhaa ambayo nimejifunza kwa miaka yote:

  1. Wasaidie kujiepusha na hali hatarishi.

    Iwe mtu unayemsaidia ni rafiki, mwenza, mwanafamilia, au kundi rika, kuwasaidia kuepuka hali hatarishi ni juhudi kubwa! Wakati wowote familia yangu inapotoka kwenda kula na mama yangu, kwa mfano, tunaomba kukaa kwenye meza iliyo mbali na baa. Ikiwa meza haipatikani, tunazungumza hadi moja ipatikane.

  2. Watetee katika hali za kijamii.

    Kwa sababu tu mtu unayemsaidia alikuwa muwazi kwako juu ya uraibu wao haimaanishi kuwa wako tayari kuuambia ulimwengu. Katika hatua za mwanzo za uponyaji, inaweza kuwa vigumu sana kuelezea kwa nini mtu anaepuka hali fulani au kufanya maamuzi fulani, hasa kwa watu wasiowafahamu. Katika hali hizi, fanya maisha yawe rahisi kwao kwa kuwasaidia kuelezea ikiwa mambo yatakuwa magumu.

  3. Wasaidie kupata rasilimali za msaada zaidi.

    Haijalishi unahusika vipi katika mchakato wa uponyaji, hakuna njia yoyote unayoweza kufanya yote. Wakati mwingine mama yangu anahitaji kuongea na mtu ambaye amewahi kuwa katika hali hiyo, mtu anayeelewa, na hiyo ni SAWA! Rasilimali za kitaalamu na vikundi vya msaada (kama vile Programu ya Uponyaji wa Uraibu ya Kanisa, vikundi vya uokoaji, wataalamu wa uraibu na tabia) kwa hakika hubadilisha maisha, kwa hivyo usisite kumuhimiza mtu unayemsaidia kunufaika kwa kutumia zana hizi.

  4. Ikiwa wataanguka, wasaidie kusimama tena.

    Ikiwa tungeishi katika ulimwengu mkamilifu, kurudia uraibu kusingekuwepo, lakini haya ni maisha ya kufa. Ikiwa mtu unayemsaidia anarudia uraibu, wakumbushe hatua kubwa waliyopiga. Watie moyo “wasikate tamaa baada ya makosa yanayofuatia na [wasijifikirie] kuwa hawawezi kuacha dhambi na kushinda uraibu.”7 Kama Mzee Ulisses Soares wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili alivyosema, “[Hawawezi] kumudu kuacha kujaribu”8 (na wewe pia vilevile). Kurudia uraibu hakuwarudishi mwanzoni. Hakufuti juhudi yote na nguvu waliyoipata. Siku zote wanakuwa na nafasi nyingine ya kurudi kwenye njia sahihi, kumfikia Mwokozi, na kuendelea kusonga.

  5. Endelea kutumaini.

    Kumwona mtu unayempenda akipambana kushinda uraibu wao wakati mwingine kunaweza kukufanya ujiulize ikiwa watapona kabisa. (Niamini, Ninajua. Nimekuwa hapo mara nyingi kuliko ambavyo ningetaka kukubali.) Hata Mormoni aliuliza: “Na ni kitu gani mtakachotumainia? Lakini haijalishi inakua ngumu kiasi gani, “tumaini kupitia upatanisho wa Kristo” daima lipo katika ufiko wetu (Moroni 7:41).

wakati wote wa maisha yangu, mama yangu ameshindwa mara nyingi zaidi kuliko ninavyoweza kuhesabu, lakini ninajivunia kusema kwamba ni miaka sita sasa tangu anywe kinywaji. Ingawa imenichukua miaka ya kujifunza na kujifunza tena jinsi ya kumsaidia vizuri zaidi, kumtazama akipona kumenifundisha kuwa hakuna mtu aliyewahi kwenda mbali zaidi. Haijalishi ni mara ngapi mtu umpendaye anarudia uraibu, endelea kusonga—endelea kuwasaidia kwa njia yoyote ile unayoweza. Kupona ni msimamo wa maisha yote—safari iliyojaa machozi, ushindi, kushindwa, na shangwe—na inafaa kuipigania.

Muhtasari

  1. Dylan Thomas, “Do not go gentle into that good night” (1951).

  2. Russell M. Nelson, “Uraibu au Uhuru,” Ensign, Nov. 1988, 7.

  3. Brené Brown, Daring Greatly: How the Courage to Be Vulnerable Transforms the Way We Live, Love, Parent, and Lead (2012), 58.

  4. Brené Brown, Dare to Lead: Brave Work. Tough Conversations. Whole Hearts (2018), 129.

  5. Russell M. Nelson, “Uraibu au Uhuru,” 7.

  6. Jeffrey R. Holland, “Iweni Wakamilifu—Hatimaye,” Ensign au Liahona, Nov. 2017, 42.

  7. Ulisses Soares, “Chukua Msalaba Wetu,” Ensign au Liahona, Nov. 2019, 114.

  8. Ulisses Soares, “Chukua Msalaba Wetu,” 114.