2020
Mpweke Wakati wa Chakula cha Mchana
Oktoba 2020


Mpweke Wakati wa Chakula cha Mchana

Mwandishi anaishi Utah, Marekani.

Kali alitaka rafiki tu.

“The Holy Spirit whispers with a still small voice” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto 105).

Picha
Lonely Lunchtime

Kali aliingia kwenye chumba cha chakula na kuangalia huko na huko. Watoto wengine wote walikimbia moja kwa moja kwa marafiki zao na kukusanyika kwenye meza. Chumba kilikuwa na kelele za sauti za kushangilia na kicheko cha furaha. Ilikuwa siku ya pili tu ya shule, lakini ilionekana kama kila mtu alikuwa na mtu wa kukaa naye isipokuwa Kali.

Aliminya mshikio wa kisanduku chake cha chakula na kwenda kwenye moja ya meza. “Naweza kukaa karibu nawe?” Kali aliuliza.

Msichana mwenye nywele ndefu, za kahawia aliangalia juu. Akapumua kwa nguvu na kutikisa kichwa chake. “Hapana. Kimechukuliwa,” alisema.

“SAWA.” Kali alikwenda kwenye kiti kingine kilichokuwa wazi na akaweka kisanduku chake cha chakula.

“Huwezi kukaa hapa! Ninahifadhi hicho kiti,” mvulana mwenye fulana ya michirizi ya kijani alisema. Alikisukuma chini kisanduku cha chakula cha Kali. Marafiki zake wote walicheka.

Kali aliinama chini na kukichukua tena kisanduku chake cha chakula. Alitembea kwenye chumba cha chakula na kukaa kwenye meza tupu. Alimwona mtu kutoka mtaani kwao na kujaribu kumpungia mkono, lakini aliangalia upande mwingine. Kali alichukia. Kwa nini hakuna ye yote aliyetaka kuwa rafiki yake?

Kali alitazama chini kwenye chakula chake. Hakutamani tena kula Alifuta macho yake, akafunga kisanduku chake cha chakula, na akatoka nje.

Kila mmoja alikuwa tayari akicheza na marafiki zake. Kali alikaa peke yake kwenye benchi na kuwatazama watoto wengine wakifurahi bila yeye. Kisha Kali aligundua kuna mvulana karibu ya umri wake amekaa peke yake kwenye nyasi. Alikuwa amevalia shati la manjano, na nywele zake zilisimama nyuma.

Kali aliangalia upande. Aliona kundi la wasichana kutoka kwenye darasa lake wakicheza miraba minne. Alitamani wangemkaribisha acheze pamoja nao.

Kali akamtazama tena yule mvulana. Kichwa chake kilining’inia chini, na alikuwa aking’oa nyasi karibu na miguu yake. Kali alikumbuka kitu fulani ambacho Mama wakati fulani alisema: Wajali watoto ambao ni wapweke.

Kali alichukia. Yeye alikuwa mpweke pia. Hakuna aliyejaribu kuwa rafiki yake!

Lakini kisha Kali alifikiria kuhusu wakati alipobatizwa mwaka jana. Aliahidi kumsikiliza Roho Mtakatifu. Labda Roho Mtakatifu alikuwa akimsaidia kukumbuka kile Mama alichomwambia. Labda Roho Mtakatifu alikuwa akijaribu kumwambia acheze na mvulana huyo mwenye shati la manjano.

Kali alishusha pumzi na kuanza kutembea. Hisia nzuri ilitawala katika moyo wake. Alitembea na kwenda kukaa karibu na yule mvulana kwenye nyasi.

“Halo,” alisema.

“Halo,” alimunyamunya.

Je, unapenda rangi gani?

“Um … kijani.”

“Hiyo ni vizuri. Mimi napenda waridi,” alisema Kali. “Je, una mnyama ye yote unayempenda?

Mvulana alikaa kwa kunyooka na kumwangalia. “Ndiyo.” Napenda sana dinosau.”

“Oh, mimi pia. Mimi napendelea triceratops.”

Mvulana alitabasamu.

Kisha kengele ikagonga. Kali alisimama na kupunga mkono wa kwaheri kwa yule mvulana. Alitabasamu alipokuwa akitembea kurudi tena darasani peke yake. Huenda asiwe na rafiki bora, lakini alijisikia furaha akijua kuwa alimfanya mtu mwingine afurahi zaidi. ●