2020
Je, Kutawaliwa na Mazoea Mabaya ni Sawa Sawa na Uasi?
Oktoba 2020


Vijana Wakubwa

Je, Uraibu ni Sawa na Uasi?

Mwandishi anaishi Texas, Marekani.

Ufahamu bora juu ya uraibu unaweza kutusaidia kuamini kuwa, siku moja, Bwana atatuokoa kutoka utumwani.

Picha
illustration of flowers

Katika ulimwengu wetu ulioanguka, uraibu ni hali ya kutatanisha na uhalisia unaobadilisha-maisha kwa wengi. Tunapotumia kitu fulani ili kuyakimbia maisha, kama vile chakula, dawa za kuandikiwa, mitandao ya kijamii, kusengenya, ponografia, uwongo, kamari, au hata mazoezi ya kupindukia, tunaweza kujikuta tukiwa tumekwama kwenye mzunguko wa uraibu.

Wakati nilipowatazama watu wazuri, wenye upendo, wanaonizunguka mimi wakipambana na uraibu —si tu kuruhusu chaguzi mbaya—nimegeukia maandiko na utafiti wa sasa juu ya uraibu ili kuelewa vyema misukumo hii ya kinyurolojia na shurutisho.

Magugu ya Uraibu

Safari ya uraibu inaweza kuwa kama kutunza bustani. Hatung’olei magugu mara moja na kutarajia kumaliza. Tunajua magugu zaidi yataota, kwa hivyo kwa uangalifu na mara kwa mara tunanang’oa magugu ili kulinda mimea.

Ikiwa tunapambana na uraibu tunaweza kukatishwa tamaa wakati tutakaporudia tena hali ile hata baada ya kutubu na kutafuta msaada. Tunaweza kushangazwa na kufadhaika kuwa majaribu haya hususani ni magumu sana baada ya nyakati za furaha au za kusikitisha sana za maisha yetu. (Kama vile magugu zaidi huwa yanakua baada ya mvua kunyesha au dhoruba nzito.)

Uraibu dhidi ya Uasi wa Makusudi

Nimegundua kuwa Shetani hutumia uraibu kama “uthibitisho” ya kuwa kwa asili sisi tunatamani maovu, kwamba tumesha hukumiwa tangu mwanzo, au kwamba Bwana amekata tamaa juu yetu. Shetani hutumia aibu kutukatisha tamaa, akisema kwamba bila kujali tunatubu mara ngapi, majaribu yanaendelea kujitokeza.

Kuna sababu nyingi kwa nini watu wanaangukia kwenye uraibu, lakini uraibu mara nyingi huanza na jaribio la kukidhi “mahitaji makubwa na yasiyofikika.”1 Kwa hivyo wakati uasi unaweza kuongoza kwenye uraibu na uraibu unaweza kusababisha dhambi, mara nyingi mazoea haya hupandwa ndani au kukuzwa katika udhaifu kuliko uasi wa makusudi.2

Kwa kushukuru, tunajua kuwa udhaifu unaweza kutupatia fursa ya kujifunza juu ya neema na kukuza imani ya kina katika nguvu za uponyaji za Yesu Kristo.3

Hadi Ukombozi kutoka Utumwani

Tunapata ufahamu wa kuongoza na kukwepa mtego wa uraibu kutoka kwa vikundi viwili vya watu kwenye Kitabu cha Mormoni: watu wa Limhi na watu wa Alma.

Makundi yote mawili yalikuwa utumwani kwa kipindi kikubwa. Wote walitambua kwamba “hapakuwa na njia yoyote ya kujikomboa wenyewe” kutoka utumwani (Mosia 21:5). Wote, baada ya muda, walimgeukia Bwana kwa ajili ya msaada.

Watu wa Limhi walikuwa utumwani kwa sababu ya uvunjifu wa sheria. Bila ya kutafuta msaada wa Bwana, walipambana na watesi wao “kwa hasira” mara tatu. Walipoteza kila pambano. Walipoanza kujinyenyekeza, “Bwana alikuwa mzito wa kusikia kilio chao … [lakini] Alisikia vilio vyao, na akaanza kulainisha mioyo ya Walamani kwamba wakaanza kupunguza mizigo yao” (Mosia 21:15; msisitizo umeongezwa). Walibarikiwa kwa unyenyekevu wao ulioongezeka, lakini “Bwana hakuonelea vyema kuwakomboa kutoka utumwani” hadi baadaye sana.

Watu wa Alma walikuwa utumwani bila kujali wema wao, lakini “walimfunulia mioyo yao [Mungu].” Hata kwa kujua tamaa zao za haki, Mungu aliruhusu muda kati ya utumwa wao na ukombozi wao. Walipoendelea kumtegemea Yeye, Aliahidi “nitawapunguzia mizigo ambayo imewekwa mabegani mwenu, hata kwamba hamtaisikia kamwe migongoni mwenu, hata mkiwa [bado] utumwani.” Kwa upande wao “walinyenyekea kwa furaha na subira kwa mapenzi ya Bwana” (Mosia 24:12, 14, 15).

Makundi yote mawili mwishowe yaliokolewa. Na sisi pia tumeahidiwa kwamba kama tutamgeukia Bwana katika utumwa wetu, “ili muwe mashahidi [Wake] hapo baadaye” na “mtajua kwa hakika kwamba, Bwana Mungu, huwatembelea watu [Wake] katika mateso yao” (Mosia 24:14)—na katika uraibu wao!

Jipe Moyo

Ikiwa unapambana na uraibu, kumbuka kuwa kwa msaada wa Bwana, wakati huu unaweza kuwa udongo wenye rutuba nzuri kwa ajili ya kukuza sifa kama za Kristo. Unapoongezeka katika unyenyekevu, utaweza kujifunza uvumilivu, huruma, subira, na upole.

kutana na viongozi wako wa ukuhani na wale wanaoweza kutoa usaidizi na, utumie nyenzo nyingi ambazo Baba wa Mbinguni ametoa ili kukusaidia kupata uhuru. Mtegemee Bwana; unapomfuata kwa bidii, Anaweza kubadilisha changamoto hii yenye kukatisha tamaa na kufadhaisha kuwa fursa nzuri ya utakaso wa kiroho.4

Mtakatifu wa Siku za Mwisho wa mwanzo kutoka Australia alipolinganisha mambo yake ya zamani na ya sasa, alisema: “Maisha yangu ya zamani [yalikuwa] nyika ya magugu, na kwa shida sana ua Lilitawanywa miongoni mwao. [Lakini] sasa magugu yamepotea, na maua Yamechipuka mahali pake.”5

Kama mimi na wewe kwa uaminifu tukipalilia bustani yetu na kumgeukia Bwana katika majaribu yetu, tutapokea ahadi iliyotolewa kwa watu wa Alma: “Shangilieni, kwani hapo kesho nitawakomboa kutoka utumwani” (Mosia 24:16).

Endelea kupalilia—mavuno yana thamani!