2020
Kusudi la Ubatizo Wangu
Oktoba 2020


Kusudi la Ubatizo Wangu

Kabla ya ubatizo wangu, nilikaa peke yangu na kuomba ili rafiki zangu waweze kutokea kimiujiza.

Picha
man sitting in chapel foyer

Kielelezo na Julia Yellow

Kama mtoto anayeishi katika vitongoji vya Taipei, Taiwan, sikuwahi kujua juu ya wamisionari. Kwa hivyo mara ya kwanza nilipokutana nao, nilikuwa na shauku ya kujua ujumbe wao. Haikuchukua muda mrefu kabla ya kutamani kufuata mafundisho yao na kuifanyia mazoezi injili katika maisha yangu. Nilihisi kuwa hii ilikuwa njia kwa ajili yangu kujua kama kweli kuna Mungu.

Ndani ya mwezi mmoja, nilikuwa nimefundishwa injili na amri ambazo zinafundishwa kabla ya ubatizo. Amani ilikuja kwangu kupitia maombi, nilipokea ufunuo binafsi kutokana na kusoma maandiko, na kamwe sikuwahi kukosa mikutano ya Kanisa. Niliamua kuwa ninapaswa kubatizwa.

Changamoto kubwa nilizokabiliwa nazo wakati huo ilikuwa shida ambazo zilikuwa zimeibuka katika uhusiano wangu na baadhi ya marafiki zangu kwa sababu walipinga kujihusisha kwangu na Kanisa. Nilisali sana juu ya shida hizi, lakini uhusiano wetu ulionekana kuendelea kuwa mbaya tu.

Niliwaalika rafiki zangu kwenye ubatizo wangu, lakini walipuuza kabisa mwaliko wangu. Hakika sikujua nini cha kufanya. Kabla ya ubatizo wangu, nilikaa peke yangu kwenye sofa lililokuwa ndani ya ukumbi wa kanisa, nikisali kwamba marafiki zangu watajitokeza kimuujiza ili niwaambie juu ya mabadiliko mazuri niliyokuwa nimefanya maishani mwangu na kuwathibitishia kuwa nilikuwa nikifanya uamuzi sahihi kwa kubatizwa.

Marafiki zangu hawakufika kabisa, lakini wakati nikimimina moyo wangu kwa Mungu, nilihisi wazo. Wakati huo, nilihisi upendo mkubwa kutoka kwa Baba yangu wa Mbinguni. Nilijua kuwa Yeye alikuwa pale na kweli amesikiliza maombi yangu.

Hapo awali nilitaka kubatizwa kwa sababu tu ya mambo mazuri ambayo yanatokea katika maisha yangu, lakini wakati huo, nilikuja kuelewa kusudi la ubatizo wangu.

Mawazo niliyopokea yalikuwa kama sauti ya Bwana ikiongea kwa upole na moja kwa moja kwangu, ikisema, “Hauhitaji kuthibitisha kitu chochote kwa mtu yeyote. Unahitaji kunithibitishia mimi tu kuwa uko tayari kuja kwangu na kuendelea kuwa mkweli kwa injili yangu kwa maisha yako yote yaliyosalia.”